USIWE NA TAMAA YA CHAKULA KINGINE.

john7

Lister
USIWE NA TAMAA YA CHAKULA KINGINE.

Hesabu 11:6 “lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu”
Nakusalimu katika jina lenye uweza la YESU KRISTO mwokozi wetu. Ni siku nyingine tena Bwana ametupa neema ya kuifikia hivyo, nakukaribisha tuyatafakari pamoja maneno yake.

Wana wa Israeli walipofika jangwani hawakujua kuwa watalishwa chakula cha aina moja tu, Mwanzoni waliifurahia ile mana, jinsi ilivyokuwa nzuri na tamu, lakini siku zilivyozidi kwenda, hamu ya mana ile ikaanza kupungua ndani yao, wakaanza kutamani na vyakula vingine..Walipoona asubuhi kifungua kinywa ni mana, mchana ni mana, chakula cha jioni ni mana.. wakasema haya mambo yataendelea mpaka lini?..wakaikinai, Wakaanza kufikiria ni wapi watapata chakula cha aina nyingine walau wabadili ladha. Ni wapi watapata nyama, watapata kuku, watapata pilau, na pizza, na Baga.

Hesabu 11:4 “Kisha mkutano wa wafuasi waliokuwa kati yao, wakashikwa na tamaa; wana wa Israeli nao wakalia tena, wakasema, N’nani atakayetupa nyama tule? 5 Twakumbuka samaki tuliokula huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu, na vitunguu saumu; 6 lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumaini isipokuwa hii mana tu. 7 Na hiyo mana ilikuwa mfano wa chembe za mtama na kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwake bedola”
Wana wa Israeli wakasau kuwa vyakula hivyo ndivyo vilivyokuwa vinawaletea magonjwa makali kule Misri, ndivyo vilivyokuwa vinafubaza miili yao. Tofauti na mana, ambayo walipoila hawakuumwa, wala kudhoofika maandiko yanasema hivyo (Kumbukumbu 8:3-4), japokuwa kilikuwa ni chakula cha aina moja tu, lakini ni salama.. Wao wakaidharau.

Ndugu yangu Mana inafananishwa na “Neno la Mungu”. Tunapookoka, tujue kuwa tutapewa chakula cha aina moja tu, nacho ni Neno la Mungu [Hilo usiliondoe akilini].. tutaamka nalo, tutatembea nalo, tutalala nalo. Ndio chakula cha Roho zetu pekee, kitufaacho kwa wakati wote hakuna kingine..Hatutalishushia na jbo lingine lolote…Hatujapewa biblia, pamoja na kitabu cha saikolojia, kitufariji Hatujapewa biblia na vilabu vya mipira (FIFA) vituburudishe , tunalimeza hivyo hivyo, bila kugoshiwa.

Lakini kwasababu ya tamaa ya mambo ya ulimwengu na mengineyo. Inasikitisha kuona wakristo wengi tunavyolikinai Neno la Mungu kwa haraka sana.. Utakuta mwanzoni mwa wokovu wetu, tulikuwa tunapenda sana kusikiliza Neno, tupo tayari kushinda muda wote kusikiliza mahubiri na mafundisho, tulikuwa tupo tayari kusoma mstari baada ya mstari, , kitabu baada ya kitabu, kudumu muda mrefu kwenye Neno la Mungu.Tukielezwa habari za mambo mengine, tuliona kama ni takataka..

Lakini ulipofika wakati tumekula tumeshiba, tunaona sasa kama hivyo vingine vya nje vinatupita.. Tunapoona biblia ni ile ile, haina matoleo mapya, maagizo ni yaleyale, yanayotutaka tuwe watakatifu na wenye imani, na tujiepushe na mambo ya ulimwengu huu.. Tunaona kama ni habari zile zile za kale za kujitesa.

Ndio hapo utamwona Mkristo anapoa anaanza, kufuatilia na miziki ya kidunia, anaanza kuwa mshabiki wa mipira na thamthilia za kidunia, tena anazichambua kwa undani kama vile tu anavyochambua Biblia, ili tu aipe nafsi yake ladha nyingine..mwingine anachanganyia na miziki ya kidunia humo humo..Mpaka Neno la Mungu linakuwa sio chakula kikuu kwake, bali sehemu ya vyakula vyake. Kama wana wa Israeli walivyoifanya mana, kuwa sehemu mojawapo ya vyakula vyao..

Lakini viliwatokea puani, wakaanza kufa, na kupata mapigo mengi sana, kutoka kwa Mungu. (Soma Hesabu 11:33).

Ndugu tunapoamua kumfuata Kristo tusitegemee tutapewa chakula kingine zaidi ya NENO LAKE. Na kama tukilikinai mapema sana, hatutamaliza mwendo wetu salama. Si ajabu tunakutwa na majaribu mengi, na mapigo mengi, kwasababu tu ya tamaa ya mambo mengine zaidi ya Neno la Mungu.

Tukijifunza kuishi sawasawa na biblia,tuitegemee hiyo tu, hata kama tutakosa vingi, hatutafaidi na vingi vya ulimwengu huu, lakini roho zetu na nafsi zetu zipo salama. Hivyo tujifunze, kukifurahia chakula hiki hiki kimoja, Mungu anatambua kuwa hatutadhoofika, kinyume chake ndio tutaimarika na kubarikiwa.

Tuache kutanga tanga na tamaa..Tii kile biblia inasema, vingine tuwaachie mataifa, Ili tuweze kufanikiwa na kuishi maisha mema katika hii dunia Mungu aliyotuweka, ndani yake.

Kumbuka shetani alilijua hilo, ndio maana alipomjaribu Bwana kule jangwani, kwa kumletea vyakula vyake vya vigeni, wakati ananjaa. Yesu alimwambia, imeandikwa mtu hataishi kwa mkate bali kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu” (Mathayo 4:1-4).

Akamfukuza, na wewe usimvulie shetani na mambo yake maovu.

Bwana atusaidie.

Ubarikiwe daima.
Whatsapp: +255693036618
 
Top