*JINSI YA KUMSIKIA MUNGU, NA KUPOKEA MAFUNUO AU JUMBE KUTOKA KWAKE*

john7

Lister
Nakusalimu katika jina kuu sana la Bwana wetu Yesu Kristo, Karibu tuyatafakari maneno ya uzima, ambayo pekee ndio yanayoweza kutufanya sisi tuwe huru kweli kweli hapa duniani( Yohana 8:32).

Leo tutajifunza, kanuni mojawapo ya kibiblia ambayo itatusaidia sisi kuweza kupokea jumbe, au mafunuo, au maarifa sahihi kutoka kwa Mungu, Imenisaidia mimi, naamini pia itakusaidia na wewe.

Kanuni ya sisi kuzungumza na Mungu, ni tofauti na ya kwake kuzungumza na sisi. Sisi tukitaka kuwasiliana naye tunachofanya ni moja kwa moja kwenda katika uwepo wake, na kupiga magoti na kupelekea haja zetu kwake, Na tukishamaliza tutanyanyuka na kuondoka na kwenda katika shughuli zetu.

Lakini Mungu, hana utaratibu huo wa kuzungumza na wewe papo kwa papo, kwa wewe ufanyavyo. Na hiyo imewafanya watu wengi wakate tamaa, pale wanapoona hakuna mwitikio wowote, kutoka upande wa pili wa Mungu.

Lakini leo tutajifunza kanuni ambayo muhimu sana kuizingatia ikiwa wewe unataka kumsikia Mungu, au kupokea mafunuo sahihi kutoka kwake.

*NA KANUNI YENYEWE NI “UTULIVU”*

Sauti ya Mungu ya kweli ipo katika utulivu, na si mahali pengine, Eliya alikuwa ni nabii ambaye Bwana anazungumza naye na kumpa taarifa nyingi, lakini hakuwahi kuisikia sauti ya Mungu vizuri, hadi siku ile alipokuwa katika utulivu, na ndio maana utaona akaufunika uso wake, alipomsikia (kuonyesha kuwa amemwona Mungu, hivyo hastahili hata kuzungumza naye). Lakini mara nyingine zote huko nyuma hakuwahi kuufunika uso wake. Utajiuliza ni kwanini? Ni kwasababu Mungu hakuwa karibu naye kama alivyomwona siku hiyo, alipokaa katika utulivu (1Wafalme 19:9-13).

Elisha alipotaka kupokea taarifa sahihi, na maagizo kutoka kwa Bwana juu ya nini yafanye yale mataifa matatu yaliyotaka kuangamizwa na taifa la Moabu,..hakukurupuka tu na kuzungumza na Bwana, bali alitaka kwanza kukaa katika utulivu, akamwita mpiga kinanda,aimbe naye nyimbo za kumsifu Mungu, ndipo taarifa sahihi zikamshukia baadaye.

2Wafalme 3:14 “Elisha akasema, Kama Bwana wa majeshi aishivyo, ambaye nimesimama mbele zake, kama singemwangalia uso wake Yehoshafati mfalme wa Yuda, singekutazama, wala kuonana nawe.

15 Ila sasa niletee mpiga kinanda. Ikawa, mpiga kinanda alipokipiga, mkono wa Bwana ukamjia juu yake.

16 Akasema, Bwana asema hivi, Fanyeni bonde hili lijae mahandaki. 17 Kwa kuwa Bwana asema hivi, Hamutauona upepo, wala hamtaiona mvua, ila bonde hilo litajaa maji; nanyi mtakunywa, ninyi, na ng’ombe zenu, na wanyama wenu.

18 Na jambo hili ni jepesi machoni pa Bwana; pia atawatia Wamoabi mikononi mwenu”.

Vilevile Mungu alipotaka kuzungumza na Musa, ili kumpa zile mbao mbili za amri na sheria yake, alimwita mlimani, , lakini utaona Musa hakwenda moja kwa moja tu,hadi kileleni bali ilimbidi asubirie chini kwa muda wa siku sita (6). Ndipo siku ya saba akasikia sauti ya Mungu ikimwita apande mlimani.

Kutoka 24:15 “Musa akapanda mlimani, lile wingu likaufunikiza mlima.

16 Na huo utukufu wa Bwana ukakaa juu ya mlima wa Sinai; lile wingu likaufunikiza siku sita; na siku ya saba akamwita Musa toka kati ya lile wingu.

17 Na kuonekana kwake ule utukufu wa Bwana kulikuwa kama moto uteketezao, juu ya mlima machoni pa wana wa Israeli.

18 Musa akaingia ndani ya lile wingu, akapanda mlimani; Musa akawa humo katika ule mlima siku arobaini, mchana na usiku”.

Kwa mifano hiyo michache ni kutuonyesha na sisi kuwa, tukitaka tumsikie Bwana, hatuna budi kuwa katika utulivu rohoni, kwamfano unapokwenda kuomba, usiishie kuzungumza tu maneno yako halafu basi unaondoka, mpe Bwana nafasi, kaa chini imba, baadaye tafakari uweza wa Mungu, soma biblia, tafakari tena, kisha rudia tena kuomba.. kwa jinsi unavyokaa sana katika uwepo wa Mungu, ndivyo unavyompa nafasi Mungu ya kushuka na kukuhudumia.

Ghafla tu utaona wingu linakushukia roho, na hapo hapo unapokea ufunuo au maarifa, au taarifa Fulani ambazo hukuwahi kuziwaza au kuzifikiri, hapo ujue tayari ni Mungu huyo, au utapokea amani Fulani, au ufumbuzi Fulani, au agizo Fulani, hapo ujue Mungu anazungumza na wewe. Lakini inahitaji utulivu wa kitambo kidogo, wakati mwingine hata masaa kadhaa. Ni kweli yapo majira utaomba tu na kuondoka, lakini yapo majira ni lazima ujiwekee muda kwa Mungu, apate nafasi ya kusema na wewe.

Vilevile, yafanya Maisha yako, yawe katika utulivu, ukiwa ni mtu wa kukesha tu mitandaoni, kuchat chat kwenye magroup, au muda wote kutazama tazama, tv au tamthilia, au muvi, miziki au michezo michezo, au kuzurura zurura, leo party hii, kesho ile.. Fahamu kuwa mambo kama hayo ni adui mkubwa sana wa Mungu kuzungumza na wewe, haijalishi utakuwa ni mwombaji kiasi gani, hutakuwa unaona mwitikio wowote kutoka kwa Mungu. Hiyo ni kwasababu haupo katika utulivu.

Kuwa mtulivu maishani, tumia muda wako, kusikiliza nyimbo za sifa kama Elisha alivyokuwa anafanya, tumia weekend zako kwenda mikesha kuomba, soma sana biblia, punguza marafiki ambao ni maadui wa Imani yako, zungumza sana Habari za Kristo, katika mazungumzo hayo utaona ufunuo unaingia ndani yake, kwasababu Kristo kashaungana nawe katika kinywa chako kama ilivyokuwa kwa wale watu wawili wa Emau (Luka 24:13)

Ukizingatia hivyo. Utamsikia, kama sio kupokea mafunuo mengi kutoka kwake, daima jiweke katika utulivu.

Bwana akubariki.

Sote tunatamani Mungu azungumze nasi, lakini tumekuwa na wasiwasi, tukadhani kuwa Mungu yupo mbali sana, na anasema tu na watumishi wakubwa, au manabii, hawezi kusema na wewe. Ukweli ni kwamba, Karama ya mtu, sio kigezo cha Mungu kuzungumza naye, haijalishi atasikia sauti, au maono, au ndoto nyingi kiasi gani. Mungu anaweza kuzungumza na kila mtu, kulingana na njia yake mwenyewe aliyotaka azungumze naye.

Japokuwa Eliya alikuwa karibu sana na Mungu, na kupokea maono mengi, na taarifa nyingi kutoka kwa Yehova, lakini hakuwahi kumsikia Mungu mwenyewe, na ndio maana hakuwahi kuufunika uso wake, maana yake hakusitiri uovu wake, alipokuwa anaongea na Mungu hadi siku ile alipokaa katika utulivu na ndio akamsikia Bwana kwa mara nyingine.,

1Wafalme 19:9 “Akafika kunako pango, akalala ndani yake. Na tazama, neno la Bwana likamjia, naye akamwambia, Unafanya nini hapa, Eliya?

10 Akasema, Nimeona wivu mwingi kwa ajili ya Bwana Mungu wa majeshi; kwa kuwa wana wa Israeli wameyaacha maagano yako, na kuzivunja madhabahu zako, na kuwaua manabii wako kwa upanga; nami nimesalia, mimi peke yangu; nao wanitafuta roho yangu, waiondoe.

11 Akasema, Toka, usimame mlimani mbele za Bwana. Na tazama, Bwana akapita; upepo mwingi wa nguvu ukaipasua milima, ukaivunja-vunja miamba mbele za Bwana; lakini Bwana hakuwamo katika upepo ule; na baada ya upepo, tetemeko la nchi; lakini Bwana hakuwamo katika lile tetemeko la nchi;

12 na baada ya tetemeko la nchi kukawa na moto; lakini Bwana hakuwamo katika moto ule; na baada ya moto sauti ndogo, ya utulivu.

13 Ikawa, Eliya alipoisikia, alijifunika uso wake katika mavazi yake, akatoka, akasimama mlangoni mwa pango. Na tazama, sauti ikamjia, kusema, Unafanya nini hapa, Eliya?”

SAUTI YA MUNGU IPO KATIKA UTULIVU.

Jambo ambalo, wakristo wa sasa tunalikwepa sana,

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,


*0789001312*
 
Top